Makala



Bila maridhiano hata 2016 hakuna Katiba

 

Rais wa Tanzania, Jakaya Kikwete, ambaye alikuwa anatamani kabla ya kumaliza muda wake wa urais kufanikisha zoezi la kupatikana kwa katiba mpya nchini. Picha na Maktaba 
Kwa ufupi
Profesa Mpangala ni miongoni mwa Watanzania waliozungumzia uamuzi wa kumaliza Bunge la Katiba Oktoba 4, mwaka huu badala ya Oktoba 31, huku upigaji kura ukisogezwa mbele hadi baada ya Uchaguzi Mkuu 2015, wakibainisha kuwa kitendo hicho ni matokeo ya ubabe wa wanasiasa wa kutotaka kukubali ushauri, licha ya kuelezwa kasoro za mchakato mzima tangu awali.

Dar es Salaam. Profesa wa Chuo Kikuu Dar es Salaam, Gaudence Mpangala amesema matatizo yanayolikumba Bunge Maalumu la Katiba yamezungumzwa na watu wengi na sasa yamegeuka wimbo wa Taifa, lakini la muhimu ni maridhiano.
Profesa Mpangala ni miongoni mwa Watanzania waliozungumzia uamuzi wa kumaliza Bunge la Katiba Oktoba 4, mwaka huu badala ya Oktoba 31, huku upigaji kura ukisogezwa mbele hadi baada ya Uchaguzi Mkuu 2015, wakibainisha kuwa kitendo hicho ni matokeo ya ubabe wa wanasiasa wa kutotaka kukubali ushauri, licha ya kuelezwa kasoro za mchakato mzima tangu awali.

Profesa Mpangala alisema, “Nilifanya utafiti na maprofesa wenzangu wawili na kuja na mapendekezo ya kusitishwa kwa Bunge hili lakini hakuna aliyetaka kusikiliza.”
Alisema kuwa hata fedha zilizotengwa sasa zimetumika bure na hata hiyo 2016 hakuna kitakachoendelea kama pande mbili zinazovutana hazitakubaliana katika mambo ya msingi. Wakili na kiongozi mwandamizi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Harold Sungusia alisema tangu mwanzo kulikuwa na vitu vitatu vilivyoonyesha wazi kuwa mchakato huo haukulenga kuwapatia Watanzania Katiba Mpya.
Sungusia alitaja vitu hivyo kuwa ni suala la Katiba Mpya kutokuwa katika Ilani ya CCM... “Kilikuwa kitu kipya na lilikuwa wazo la Rais Jakaya Kikwete. Kumbuka mwanzoni CCM haohao walisema hakuna haja ya kuandika Katiba na ndiyo haohao wako bungeni wakibadilisha Rasimu watakavyo.

“Pili, Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ilikuwa na kasoro nyingi. Sheria hii iliandaliwa kwa ajili ya kutopata Katiba Mpya. Walibadilisha Kifungu cha 36 na kukiweka katika sheria ya kura ya maoni ambayo sasa inaeleza kuwa iwapo watakaopiga kura hawatazidi nusu kwa mara mbili, unaanza mchakato upya.”
Alisema kasoro ya tatu ni kuchanganya majukumu ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba na Bunge Maalumu la Katiba na kusisitiza kuwa hakukuwa na ulazima wa kuwapo na vyombo hivyo viwili kwa wakati mmoja kwa kuwa kimoja tu kingetosha kutengeneza rasimu.
Mwenyekiti wa Asasi za Kiraia (Azaki), Irenei Kiria alisema, “Rasimu iliyotolewa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba ilitakiwa kupelekwa katika kura ya maoni moja kwa moja, kitendo cha kuipeleka bungeni ilikuwa ni kupoteza muda.”
Kiria alisema hata utungaji wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ulikuwa na tatizo kutokana na kuruhusu wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano kuwa wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba.
“Tangu mwanzo hakukuwa na nia ya kupata Katiba Mpya. Bunge hili lilitakiwa kuahirishwa tangu siku ambayo Rais Kikwete alitoa hotuba yake ya kufungua Bunge hilo maana alionyesha wazi kuwa CCM haitaki Katiba Mpya.”

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni