Alhamisi, 11 Septemba 2014

unyama wa kutisha



UNYAMA WA KUTISHA GEITA
WANAFUNZI WATATU WAUAWA  KULIPA KISASI CHA WAZAZI WAO
Baba,mama yao na dada hali zao ni mbaya
Na Eliud Dalei,Geita 07/09/2014
WAKATI familia za askari wawili wa kituo cha polisi Bukombe waliouawa na majambazi usiku wa kuamkia septemba 6 zikiendelea kuomboleza,mauaji mengine ya kinyama yamefanyika wilayani Geita baada ya watu wasiojulikana kuwachomea ndani ya nyumba wanafunzi watatu walioteketea na miili yao kubaki mmajivu.
Tukio hilo la kikatiri  linalodaiwa kufanywa na mtu aliyekuwa na ugomvi na familia hiyo, limetokea usiku wa kuamkia septemba 7 saa 8, katika mtaa wa elimu,kata ya kalangalala Wilayani Geita mkoani Geita.
Akizungumza na gazeti akiwa eneo la tukio ofisa mtendaji wa kata ya kalangalala mjini Geita Hamad Husein amedai kuwa, tukio hilo linadaiwa kufanywa na mtu aliyekuwa na ugomvi na familia hiyo uliotokana na mgogoro wa kiwanja.

 
Hamad bila kumtaja mtu huyo kwa madai ya kutokuvuruga ushahidi kabla mhusika huyo hajakamatwa alisema,mtu huyo amefikia hatua hiyo ya kuichomea ndani ya nyumba familia hiyo na kusababisha vifo vya wanafunzi hao na wengine kujeruhiwa baada ya kuona haki yake ya kupata eneo hilo ikicheleweshwa.
Husein amewataja wanafunzi walioungulia kwenye nyumba hiyo kisha kupoteza maisha kuwa ni pamoja na Regnard Robert(9)mwanafunzi wa darasa la nne katika shule ya msingi ukombozi,Sofia Robert(6)wa darasa la kwanza ukombozi  na Remijus Robert(4)mwanafunzi wa darasa la awali zote zikiwa katika mtaa wa elimu Nyankumbu Geita.
Husein amefafanua kuwa,mbali na miili ya wanafunzi hao kuteketea kwa moto na miili yao kubaki majibu,hali za wazazi wa watoto hao akiwemo dada yao mkubwa ni mbaya na wamekimbizwa katika hospitali ya wilaya ya Geita kwa matibabu zaidi.
Amewataja majeruhi hao kuwa ni pamoja na Robert Remijus(baba wa familia hiyo),Angelina Gaspar(mama wa familia) pamoja na Scholastika Robert(15)ambaye  dada wa marehemu hao anayesoma kidato cha pili katika shule ya sekondari mwatulole iliyopo kitongoji cha mwatulole katika kata ya kalangalala mjini Geita.
Kwa mjibu wa Husein tayari amewasiliana na jeshi la polisi wilaya ya Geita na wameanza msako wa kumtafuta mtu anayedaiwa kuhusika na tukio hilo hilo na kuwaomba wananchi kutoa ushirikiano wa dhati ili kufanikisha kumkamata kisha kumfikisha kwenye vyombo vya sheria kujibu tuhuma zinazomkabili.
Kwa upande wao mwenyekiti wa mtaa huo wa elimu Hassan Mshola pamoja na mtendaji wa mtaa huo Ally Semfukwe mbali na kulaani vikali mauaji hayo yaliyotokea kwenye ubalozi wa mchungaji Jonas, wameahidi kufanya kila iwezekanavyo mtu aliyefanya ukatiri huo anakamatwa mara moja.
Aidha katika tukio hilo mmoja wa watoto wa familia hiyo King Robert(13)hakuwepo wakati nyumba yao ikiteketezwa kwa moto na kusababisha vifo hivyo baada ya siku hiyo kulala kwa bibi yake(nyanya)kitongozi cha magema nje kidogo ya tukio hilo.
Mganga mfawidhi katika hospitali ya wilaya ya Geita Dr Adam Sijaona amekiri kupokea sehemu ya miili ya wanafunazi hao walioteketea kwa moto na imehifadhiwa katika chumba cha maiti cha hospitali hiyo.
Dr Sijaona amefafanua kuwa,majeruhi mmoja kati ya watatu ambaye ni Scholastika amepewa rufaa ya kwenda katika hospitali ya rufaa ya Bugando ya jijini mwanza kutokana na hali yake kuwa mbaya huku wazazi wao wakibaki katika hospitali hiyo wakiendelea kupatiwa matibabu.
Kwa mjibu wa Dr Sijaona,baba na mama wameungua sehemu za usoni,mikononi na miguuni huku binti yao aliyehamishiwa Bugando akiungua mwili mzima.
MWISHO.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni