Alhamisi, 2 Julai 2015

GEITA WATINGA NA CHANDARUA KWENYE KITUO CHA BVR

NA VICTOR BARIETY,GEITA 26/06/2015

UPUNGUFU wa vifaa vya uandikishaji kwenye zoezi la kuandikisha wananchi kwenye daftari la kudumu la wapiga kura kwa mfumo wa BVR linaloendelea katika halmashauri ya mji wa Geita limechukuwa sura mpya baada ya baadhi ya vijana kuamua kwenda na chandarua vituoni huku kinamama wenye watoto na wajawazito wakidai kubaguliwa kwa madai kuwa kiherehere chao kimesababisha hali walizonazo.


                                 WAKAZI WA GEITA WAKIWA NA VYANDARUA KWENYE
                                VITUO VYA BVR KAMA       WALIVYONASWA NA MPIGAPICHA WETU


Hali hiyo imejitokeza jana(juzi)kwenye baadhi ya vituo vya shule za msingi Kalangalala na Mtakatifu Aloyce inayomilikiwa na kanisa katoliki jimbo la Geita.

Mwandishi wa habari hizi alifika katika kituo cha shule ya msingi Kalangalala na kushuhudia baadhi ya vijana wakiwa kwenye foleni ya kuandikishwa huku wakiwa wamebeba chandarua wakijiandaa kulala kwenye kituo hicho iwapo watakosa fursa ya kujiandikisha kwa siku hiyo ili kuwahi foleni siku inayofuata.

Kwenye kituo cha shule ya msingi Mtakatifu Aloyce baadhi ya kinamama wenye watoto na wale wajawazito mbali na kuamka alfajiri lakini hadi kituo kinafungwa majira ya jioni walikuwa hawajapata fursa hiyo wakidai wanasukumwa na kutishiwa kupigwa na baadhi ya vijana wakielezwa kuwa kiherehere chao kimepelekea wapate ujauzito na watoto na kutakiwa kupanga foleni kama wao.

Mmoja wa akina mama wajawazito Anastazia James(28),mkazi wa mtaa wa Tambukaleli katika kata hiyo,alidai kuwa pamoja na kuamka alfajiri hadi majira ya jioni hakupata fursa ya kuandikishwa kutokana na kusukumwa akitakiwa kupanga foleni kwa madai hawawezi kuruhusu aliyepata ujauzito kwa kupenda apewe fursa hiyo kama sheria inavyosema.

‘’Nimefika hapa kuanzia saa 11 alfajiri lakini mpaka sasa sijaandikishwa na nikitaka kuingia kwenye chumba cha uandikishaji nasukumwa na kutishiwa kupigwa na kwa hali niliyonayo ya ujauzito siwezi kuhimili kusimama kwa muda mrefu naomba serikali itusaidie maana kwa hali ilivyo zoezi litamalizika bila sisi wajawazito kupata fursa’’alisema.

Naye Jastina Izilael(23),mkazi wa mtaa huo alisema pamoja na kituo hicho kubandikwa matangazo yanayotoa fursa kwa akina mama wenye watoto,wajawaziti,walemavu na wajawazito hali imekuwa tofauti maana wao wanabaguliwa.

‘’Nimefika hapa usiku wa kuamkia leo(juni 15),na nimekuwa kama mtu wa kumi kufika kituoni lakini pamoja na kukuta mabango yameandikwa wajawazito,walemavu,wazee na sisi wenye watoto tunapewa fursa ya kujiandikisha hali imekuwa tofauti na kama unavyoona mpaka sasa kituo kinafungwa sijajiandikisha na siyo mimi tu unaweza kuona wajawazito na wenye watoto tulivyo wengi kituoni,tunaomba tusaidiwe jamani’’alilalama.

Mwenyekiti wa mtaa huo,Mabula Ndoshi akizungumza na kinamama hao nje ya kituo hicho aliwatoa hofu na kuwaahidi kuwa kadiri siku zinavyokwenda watahakikisha wanaandikishwa.

Alidai hali hiyo imetokana na ubovu wa mashine za BVR kuwa mbovu ambapo badala ya zoezi hilo kuanza asubuhi lilianza mchana kutokana na mashine hizo kuharibika.

‘’Nataka niwahakikishie tu kwamba,hii vurugu ni kwa sababu mashine ni mbovu ila tumeongea na mkurugenzi amedai kuanzia kesho mashine zitaongezwa na wote mtaandikishwa’’alisema Ndoshi.

Kwa upande wa Mtaa wa Msalala road hali ilikuwa vivyo hivyo ambapo pamoja na mtaa huo kuwa na watu 3500 wenye sifa za kupiga kura mashine ilikuwa moja na kusababisha msongamano mkubwa wa watu.

Mwenyekiti wa mtaa huo,Elineema Mafie aliitupia lawama ofisi ya mkurugenzi wa halmashauri ya mji wa Geita kwa kuharibu zoezi hilo kana kwamba walifanya kwa kulazimishwa.

‘’Mtaa wangu unawatu 3500 wenye sifa za kuandikishwa,na mashine moja inao uwezo wa kuandikisha watu 140 kwa siku,na zoezi hili limeanza leo(jana) juni 25 na linamalizika julai 1,kwa hiyo ukifanya hesabu kwa siku hizo watakaoandikishwa ni watau 980 tu na hawa wengine 2,520 inamaana hawatapata fursa ya kuandikishwa’’

‘’Mi nafikiri serikali kupitia tume ya uchaguzi haikuwa na lengo la kuandikisha watu ndiyo maana ukiangalia zoezi hili linavyokwenda ni kama wamelazimishwa maana hata mkurugenzi wa halmashauri ya mji hajashirikisha viongozi wa mitaa husika na linapelekwa kibubububu tu,labda nyie waandishi mtusaidie’’alisema Mafie.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya mji wa Geita Hellen Kahindi alipotakiwa kuzungumzia changamoto hizo alidai kuwa kadiri siku zinavyokwenda wanatatua baadhi ya changamoto hizo na kuwahakikishia wananchi kuwa kila mmoja lazima ataandikishwa.

Kwa mjibu wa Kahindi,zoezi hilo lililoanza juni 25 kwenye kata za mjini Kalangalala na Nyankumbu,linatarajiwa kukoma juali 1 mwaka huu ikiwa ni awamu ya tatu na ya mwisho katika halmashauri hiyo baada ya awamu ya kwanza na ya pili iliyoanza juni 9 hadi 23,mwaka huu kumalizika kwenye kata za Shiloleli,Bulela,Bung’hwangoko,Nyanguku,Ihanamilo,Buhalahala na Mtakuja zilizo nje na mji wa Geita.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni