Ijumaa, 12 Septemba 2014

GEITA WAIWEKA KAMATI KUU YA CHADEMA TAIFA,MSALABANI

GEITA WAIWEKA KAMATI KUU YA CHADEMA TAIFA,MSALABANI!

Na Eliud Dalei,Geita 11/09/2014
BAADHI ya wapenzi na wanachama wa chama cha Demokrasia na maendeleo(CHADEMA),Mkoa wa Geita wenye mapenzi mema na chama hicho wameishauri kamati kuu ya chama hicho Taifa ambayo imepewa jukumu la kuthibitisha majina ya makatibu wa jimbo,wilaya na mkoa kufanya maamuzi magumu kwa kuwaondoa kwenye nafasi hizo baadhi ya wateule wa nafasi hizo wasio na sifa.





Pia wanachama hao wameuomba uongozi wa chama hicho Taifa kuwaondoa kwenye nafasi zao baadhi ya wagombea waliochaguliwa kushika nyadhifa mbalimbali kwenye chama hicho hasa wale waliopita kwa harufu ya rushwa kinyume cha katiba ya chama chao.

Wanachama hao wamefikia hatua hiyo baada ya kugundua kuwa wateule wa nafasi hiyo ngazi ya wilaya na mkoa wa Geita walipitishwa kwenye nafasi hiyo kimizengwe mbali na kutokuwa na sifa za kuweza kuimudu.

Wateule kwenye nafasi hizo wanaodaiwa kupitishwa kimizengwe,kwa upande wa katibu wa wilaya ya Geita ni Rogers Luhega ambaye awali alikuwa katibu wa jimbo la Geita kabla ya nafasi yake kuchukuliwa na Mutta Robert ambaye kitaaluma ni mwanasheria,huku nafasi ya katibu wa mkoa wa Geita ikichukuliwa na Sudi Tanyagara.

Sababu za wanachama hao kuitahadharisha kamati kuu kufanya maamuzi magumu ili kukinusuru chama hicho kwa kuwaondoa kwenye nafasi hizo wateule hao ni pamoja na mienendo yao inayotia shaka  ndani ya chama inayoashiria kukivuruga chama hicho wakati huu wa kuelekea kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa pamoja na uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.

Pamoja na mambo mengine,wanachama hao wameonyeshwa kukerwa na kauli aliyoitoa Katibu mteule wa chama hicho Mkoa wa Geita Sudi Tanyagara muda mfupi baada ya kutangazwa mshindi kauli waliyodai ikifumbiwa macho inaweza kukisambaratisha chama hicho.

Tanyagara huku akirekodiwa na mitambo ya JAMUHURI,akigeuka kituko ukumbini baada ya kutangaza hadharani kuwa katika uongozi wake hatafuata katiba ya chama hicho kutatua migogoro mbalimbali jambo lililotafsiliwa kuwa iwapo kiongozi huyo atathibitishwa rasmi na kamati kuu,uongozi wake utakuwa wa kidikiteta usiojali utu wa mwanadamu na misingi ya kidemokrasia.

Chanzo cha katibu huyo kutoa kauli hiyo,ni baaada ya baadhi ya wajumbe wa mkutano huo kupendekeza wagombea wawili kati ya watano Neema Chozaile na Julius Marco warudiwe kupigiwa kura kwenye nafasi ya uenyekiti BAWACHA mkoa wa Geita kwa kuwa mshindi katika nafasi hiyo Chozaile hakufikisha 50 asilimia kama katiba ya chama hicho inavyosema.

‘’Mheshimiwa mwenyekiti katiba ya chadema toleo la 2006 ibara ya 6.3.1(C) inasema majina ya wagombea wote wenye sifa zinazotakiwa watapigiwa kura ya siri na kikao kinachohusika na mshindi atapatikana kwa wingi wa kura usiopungua 50 asilimia ya wapiga kura halali waliohudhuria kikao cha uchaguzi na kwa kuwa kwenye nafasi ya uenyekiti BAVICHA mshindi(Chozaile)hajafikisha hiyo asilimia tunaomba warudie kupigiwa kura’’alisikika mjumbe mmoja akishauri.

Hata hivyo katika hali isiyotarajiwa Katibu mteule wa Chadema Mkoa wa Geita Tanyagara alisimama na kupinga mapendekezo hayo kwa kile alichodai katiba haiko juu ya wadhifa alionao na kumtaka mwenyekiti afunge kikao watu warudi majumbani mwao.

‘’Nasema hivi hakuna cha katiba inasemaje,mimi ndiyo katibu wa mkoa wa Geita hapa uchaguzi haurudiwi,mimi kama katibu nimesema na katika uongozi wangu sintokubali katiba ya chama itawale maamuzi yangu mwenyekiti naomba ugunge kikao na kama kuna mtu hajaridhika atakata rufaa kwangu’’alifoka Tanyagara na kusababisha ukumbi mzima kulipuka ukiashiria kupinga udikteta wake.

Kufuatia hali hiyo,mwenyekiti mteule wa Chadema Mkoa wa Geita Alphonce Mawazo akionyesha kukerwa na kauli hiyo alisimama akitaka kuwatuliza wajumbe lakini msimamizi wa uchaguzi huo Cosmas Makune alimsihi akae chini na msimamizi aliamua kufuata katiba kwa kurudia uchaguzi wa nafasi hiyo na Chozaile kuibuka tena mshindi.

Kwa mjibu wa wapenzi na wanachama wa chama hicho ambao wamekuwa wakifuatilia nyendo za kiongozi huyo walidai kuwa,hiyo haikuwa mara ya kwanza kwa katibu huyo kufanya maamuzi kidikiteta,katika uchaguzi wa jimbo la Busanda Geita Tanyagara akiwa msimamizi wa uchaguzi huo uliofanyika Agost 10 mwaka huu kwenye nafasi ya uenyekiti alimtangaza mshindi wa nafasi hiyo pamoja na kura kuzidi wapiga kura.

Wagombea kwenye nafasi hiyo walikuwa watatu,na wapiga kura 109,ambapo George Kwacha kura 46,Julius Marco 44 na Joseph Butondo 21 ambapo idadi ya wapiga kura inakuwa 111 lakini alimtangaza Kwacha kuwa mshindi badala ya uchaguzi kurudiwa.

Vivyo hivyo kwenye nafasi ya ukatibu wa jimbo hilo ambapo Vedastus Mtasigwa alipata kura 48,Deogratius Sangalali 60 na kura 1 iliharibika lakini aligoma kumtangaza mshindi kwa kuwa aliyeshindwa ni rafiki yake wa karibu.

Hali hiyo imezidi kuwashitua baadhi ya wanachama wa chama cha hicho na kuiomba kamati kuu ya chama hicho Taifa kutomthibitisha katika nafasi hiyo kwa kuwa ameonekana hana sifa za kiuongozi.

Kwa upande wa Luhega,wanachama hao wamedai hana sifa za kukiondoa chama hicho kilipo kutokana na walichodai hata alipokuwa katibu wa jimbo la Geita alishindwa kuwaunganisha wanachama na badala yake alizalisha makundi ambayo yalikwishaanza kukitafuna chama hicho.

Pia walidai hata nafasi yake aliipata kwa kubebwa na msimamizi wa uchaguzi huo Njugu Tungaraza aliyemtangaza kuwa katibu mpya  wa wilaya ya Geita mbali na wajumbe wa mkutano huo kumpigia kura 9 za hapana kati ya kura 16 katika  uchaguzi uliofanyika Agost 29 mwaka huu.

Kituko hicho cha uvunjaji wa katiba na miongozo ya uchaguzi kilitokea ndani ya ukumbi wa Hotel ya kisabo mjini Geita katika mkutano mkuu wa uchaguzi wa mabaraza na viongozi wa wilaya wa chama hicho.

Wagombea katika nafasi hiyo walikuwa wawili Mapesi Maagi na Rogers Luhega na katika kile kinachoonyesha zoezi hilo lilitawaliwa na mianya ya rushwa msimamizi wa uchaguzi huo Njugu Tungaraza aliondoa jina la Maagi dakika za majeruhi ukumbini hapo ili Luhega apite bila kupingwa.

Hali hiyo ilipelekea wajumbe wa mkutano huo kucharuka wakihoji sababu za Maagi kuenguliwa bila majibu ya kuridhisha zaidi ya kuambulia vitisho kutoka kwa Tungaraza.

Hata hivyo katika kile kilichoonyesha hasira za wajumbe hao hata baada ya kuweka jina moja la Luhega katika kinyang’anyiro hicho ili lipigiwe kura za ndiyo na hapana kura zilizopigwa nyingi zilikuwa za hapana lakini haikumzuia msimamizi kumtangaza Luhega kuwa mshindi wa nafasi hiyo.

Kura zilizopigwa zilikuwa 16 na kati ya hizo Luhega ambaye hata hivyo hakuwepo katika uchaguzi huo alipigiwa kura 9 za hapana na 7 za ndiyo lakini msimamizi aliamua kumtangaza kama mshindi huku akijitetea kuwa,amefanya hivyo kwa lengo la kupunguza makundi ndani ya chama.

‘’Inakuwa siyo vizuri mtu aliyekuwa kwenye system leo aondolewe hivi hivi...huyu alikuwa katibu wa chama jimbo la Geita na ameshindwa kwenye nafasi hiyo nah ii nayo mnataka mmuondowe..ndiyo maana nimeamua kuondoa jina la Maagi ili apite bila kupingwa na kwa kuwa mmempigia kura za hapana mimi namtangaza mshindi kwenye nafasi hiyo na ambaye hajaridhika anaweza kukata rufaa’’alisikika Tungaraza akitamba na kuwaacha wajumbe wa mkutano huo midomo wazi wasijuwe la kufanya.

Aug 11 mwaka huu kabla ya kupewa nafasi hiyo kwa kura za hapana  Kamati kuu ya Chadema ilimvua Luhega wadhifa wa ukatibu wa jimbo kwa tuhuma za kutumia madaraka yake vibaya,ikiwa ni siku moja  baada ya yeye na  kamati yake tendaji ya jimbo kumvua uanachama Diwani wa viti maalumu(Kagu), Maliselina Simbasana ambapo piqa  amekuwa akituhumiwa kumuunga mkono mbunge wa Kigoma kaskazini Zitto Kabwe pamoja na kwamba amekuwa akikana tuhuma hizo.
Kufuatia hali hiyo, Katibu wa wazee wa chama hicho Amos Nyanda alipewa na  uongozi wa kanda jukumu la kuratibu na kusimamia chaguzi zote baada ya viongozi wa jimbo akiwemo Luhega kukosa sifa ya kufanya hivyo.
Hii si mara ya kwanza kwa Luhega kutumia madaraka yake vibaya ambayo kwa kiasi kikubwa yamekiathiri chama hicho.
Julai 27 aliamua kuufuta uongozi wa kata ya kalangalala na mabaraza yote ya chama hicho kwenye kata hiyo.
Uchaguzi huo wa Mabaraza ulifanyika baadaye kwa agizo kutoka kamati kuu ya chadema Taifa chini ya uratibu wa Nyanda ulifanyika Aug 14 ukisimamiwa na viongozi wa kanda ya ziwa magharibi.
Kituko kingine alichofanya msimamizi huyo,pia kwenye nafasi ya mkutano mkuu wa Taifa wagombea wawili kati ya 6 waliokuwa wakiwania nafasi hiyo waligongana kura lakini msimamizi aliamuru mwenyekiti wa kikao hicho aliyemteuwa yeye(msimamizi),kupiga kura ya turufu kwa mmoja wa wagombea ili kumpa ushindi kinyume cha taratibu za uchaguzi.

Aliyepigiwa kura ya turufu na mwenyekiti wa kikao hicho na kupatiwa ushindi wa upendeleo ni Aloyce Shigela(Mtafiti wa nyaraka na utafiti wa Chadema Mkoa wa Geita)cheo ambacho pia hakiko kikatiba  aliyekuwa akichuana na Daud Ntinonu.

Wengine walioenguliwa kimizengwe ni Sophia Ludandali aliyekuwa ameomba nafasi ya uenyekiti wazee wilaya ya Geita na badala yake nafasi hiyo alipewa Amosi Nyanda kwa kubebwa aliyekuwa ameomba ukatibu wazee Wilaya.

Pia Beatrice Maganga aliyekuwa ameomba ukatibu wa wanawake Wilaya naye alienguliwa kwenye kinyang’anyiro hicho dakika za majeruhi na nafasi hiyo kuachwa wazi bila sababu za msingi lengo likielezwa ni kudhoofisha kambi inayomuunga mkono mwenyekiti wa chadema Taifa Freeman Mbowe na kuimalisha kambi ya Luhega ambayo imekuwa ikiunga mkono harakati za  Zitto Kabwe.

Tayari wagombea wote ambao wamefanyiwa mizengwe kwenye nafasi walizoomba wamekata rufaa ngazi husika wakipinga msimamizi huyo kuendesha zoezi hilo kibabe bila kujua kwa kufanya hivyo ni kukiathiri chama chao.

Pia Husna Amri ambaye ni mratibu wa BAWACHA Mkoa wa Geita na ambaye amefanikiwa kutetea nafasi hiyo,anatuhumiwa kupita kata 11 kati ya 22 za wilaya ya Chato Mkoa wa Geita akiwahadaa akina mama kumchagua kwa madai kuwa amepewa fungu(pesa)na  Josephine Mushumbusi kwa ajili ya kuwawezesha wanawake kwenye  vikundi vyao vya ujasiliamali.

Mshumbusi ni mke wa katibu mkuu wa chama cha demokrasia na maendeleo(CHADEMA),Dr Wilbrod Slaa na kuwaahidi watakapomchagua atawagawia pesa hizo kwa ajili ya kujikwamua kiuchumi.

Kwa mjibu wa Husna vikundi hivyo vilipaswa kuundwa na wanawake wasiopungua 30 hali ambayo kwa sasa imejenga chuki baina ya wanawake hao na Mshumbusi baada ya kubaini ilikuwa janja nyani ya kujinadi ili kujipatia kura kupitia mgongo wa mke huyo wa Dr Slaa.
Baadhi ya kata alizohadaa wanawake hao ni pamoja na Bwanga,Buziku,Bukome,Makurugusi,Butengolumasa,Buseresere na Bwela.

Baadhi ya viongozi wa kata hizo akiwemo Josephat Manyenye kutoka kata ya Bwela anakiri Amri kupita kwenye kata hizo na kuwahadaa baadhi ya kina mama na yeye baada ya kumfuma akifanya hivyo alimtimua kwenye kata yake huku akimuonya kutokanyaga tena maeneo hayo kabla na baada ya uchaguzi huo uliomweka madarakani.

Kwa sasa Husna ndiye mratibu wa BAWACHA wa chama hicho Mkoa wa Geita baada ya kufanikiwa kuwahadaa kinamama hao na alichaguliwa Agosti 30 mwaka huu  na wenyeviti wa BAWACHA kutoka kwenye majimbo yote ya Mkoa wa Geita.

Mshumbusi alipotafutwa kwa njia ya simu ili kutoa ufafanuzi wa suala hilo iwapo alimtuma kufanya hivyo simu yake ilikuwa haipatikani na gazeti hili linaendelea kumtafuta na mahojiano yake yatapewa uzito wa kipekee kwenye gazeti hili ili jamii wakiwemo kinamama hao wafahamu kile alichokisema.

Hata hivyo Amri alipopigiwa simu na gazeti hili Septemba 5 mwaka huu saa 13:26 na kuongea kwa sekunde 00:00:57 badala ya kutoa ushirikiano aliporomosha matusi ya nguoni kwa mwandishi wa habari hizi na mengine hayawezi kuandikika.

‘’We mse.......nini.......nitolee upumbavu wako hapa’’alifoka Amri kisha kukata simu.

Kada mwingine wa chadema anayedaiwa kukivuruga chama hicho ni Neema Chozaile,ambaye ni mwenyekiti wa BAVICHA Mkoa wa Geita aliyechaguliwa hivi karibuni katika uchaguzi uliofanyika Agost 30 mwaka huu.

Pamoja na mambo mengine,Chozaile anatuhumiwa kama kinara wa vurugu zilizotokea kwenye uchaguzi  wa viongozi wa chama na mabaraza ya(CHADEMA)katika kata ya Kalangalala mjini Geita zilizopelekea mwenyekiti wa Mtaa wa Tambukaleli kupitia chama hicho kujeruhiwa vibaya mdomoni na mgongoni.

Tukio hilo lilitokea Agost 14 mwaka huu majira ya saa 6:46 mchana muda mfupi baada ya wasimamizi wa uchaguzi huo kutoka kanda ya ziwa magharibi kuwasili eneo la uchaguzi huo amabo awali ulitakiwa kufanyikia kwenye ukumbi wa ofisi ya serikali ya mtaa wa Mkoani inayoongozwa na Chadema.

Mapema asubuhi kabla ya ugeni huo kuwasili eneo hilo hali ya usalama na utulivu ilikuwa imetanda huku wananchama wa chama hicho wakiwa wamekaa makundi wakibadilishana mawazo na kila mmoja akiwa na shauku ya uchaguzi huo.

Hata hivyo katika hali isiyokuwa ya kawaida katibu wa mwenyekiti wa mtaa huo wa Mkoani,Peter Donald(CHADEMA)alifika eneo hilo kisha kufunga ukumbi uliokuwa umeandaliwa kwa ajili ya mkutano wa uchaguzi akidai kufanya hivyo kutokana na maagizo aliyopewa kutoka juu kisha kuondoka eneo hilo akiwaacha wanachama wa chama hicho wakiwa wameduwaa.

Majira ya saa 6:23 wasimamizi kutoka kanda waliwasili eneo hilo wakiwa na gari namba T 156 CDA aina ya Ranger Ford na kuelezwa kuwa ukumbi wa chama chao uliokuwa umeandaliwa kwa ajili ya kikao ulikuwa umefungwa kwa maelekezo ya aliyekuwa katibu wa jimbo hilo kabla ya kuvuliwa madaraka Rogers Luhega akishirikiana na mwenyekiti wa mtaa huo Peter Donald ambaye pia ni diwani ya kata hiyo kupitia chama chao.

Wakati ugeni huo ukipata maelezo hayo lilitokea kundi la wanachama wa chama hicho linalomuunga mkono Luhega kisha kuvuruga maongezi hayo na kuanza kuporomosha matusi ya nguoni kwa wasimamizi hao kutoka kanda na kwa baadhi ya viongozi wa chama hicho akiwemo Daud Ntinonu aliyedhalilishwa kwa kila aina ya matusi lakini hakujibu lolote.

Kundi hilo lililokuwa likiongozwa na baadhi ya viongozi wa Chadema akiwemo Neema Stephen Chozaile(Mratibu Bavicha Mkoa wa Geita),Elikana Gidion(Katibu mwenezi tawi la Nyanza),Peter Mazura(bodigadi wa kujitegemea wa Luhega),Sospiter Sweya(Mwenyekiti tawi la mwatulole)
Tom Revons(Katibu tawi shilabela),Fikiri Charles Toi(Mwenyekiti kata ya kalangalala aliyejihudhuru)na Albert Machumu pamoja na mambo mengine lilijiapiza kuwa liko tayari kupoteza maisha lakini si kushuhudia uchaguzi huo unafanyika.

Wakati hayo yakiendelea wasimamizi wa uchaguzi huo walikuwa kimya wasijue la kufanya na baada ya muda kundi hilo lilibeba mawe na kuanza kuwashambulia wenzao na moja likatua mdomoni na mgongoni kwa mwenyekiti wa mtaa wa Tambukaleli Mabula Ndoshi aliyejeruhiwa vibaya.

Kufuatia hali hiyo baadhi ya wanachama walitimua mbiyo huku dereva wa gari lililokuwa limebeba wasimamizi hao akitumia uzoefu wake kwa kuwabeba viongozi hao kisha kuliondosha kwa kasi gari hilo ambalo liliokolewa na Redbrigade wa chama hicho waliofika eneo hilo mara moja kisha kuwadhibiti kundi lililoleta vurugu ambalo nalo lilitimua mbio kukwepa mkong’oto kutoka kwa vijana hao wa ulinzi wa chadema.

Vurugu hizo zilitulia majira ya saa 7:40 na msamalia mmoja wa eneo hilo alitoa ukumbi na uchaguzi ukaendelea kwa amani ambapo hata hivyo baada ya kura kupigwa uongozi wote wa kata hiyo chama na mabaraza uliokuwa umefutwa kimizengwe na aliyekuwa katibu wa chama hicho jimbo la Geita,Luhega ulichaguliwa kwa mara nyingine tena.


Siku moja kabla ya uchaguzi huo aliyekuwa  katibu wa chama cha demokrasia na maendeleo(CHADEMA),jimbo la Geita,kabla ya kuvuliwa wadhifa huo na kamati kuu ya Chadema Taifa  Luhega na anayedaiwa kuwa kambi ya mbunge wa kigoma kaskazini Zitto Kabwe aliapa kuzuia huo uchaguzi wa kata na wa jimbo usifanyike mbali na maagizo hayo kutoka kamati kuu Taifa ya Chadema iliyoagiza uchaguzi huo ufanyike ndani ya wiki hii tambo ambazo hata hivyo ziligonga ukuta na chaguzi zote hizo zikafanyika.

Kabla ya kufanyika kwa chaguzi hizo baadhi ya  wanachama wa cha Demokrasia na Maendeleo Chadema wa kata ya Kalangalala mjini Geita walirushiana ngumi wakituhumiana kuchukua rushwa kuvuruga uchaguzi wa kata hiyo sakata  lililotokea saa 1 jioni kwenye Hoteli ya Wandela Mjini Geita,baada ya kundi la Luhega wakiwemo baadhi ya wagombea wa nafasi mbalimbali wa kata na jimbo kukutwa likipanga njama chafu za kuhujumu uchaguzi huo.
Mwisho.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni